Sunday, June 20, 2010

Mwandosya ahujumiwa na wana CCM wenzake?


NYARAKA za siri zinazoonyesha mpango wa kumtokomeza kisiasa Waziri wa Maji na Umwagiliaji, Profesa Mark Mwandosya zimevuja.

MwanaHALISI limepata nyaraka hizo zinazomtaja mkuu wa mkoa wa Mbeya, John Mwakipesile na viongozi wengine wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kuwa katika njama hizo.


Katika andishi rasmi, Mwakipesile anasema kwamba anatuhumiwa kushirikiana na mbunge wa Igunga, Rostam Aziz na swahiba wake mkuu, Waziri mkuu aliyejiuzulu, Edward Lowassa kumwangamiza Mwandosya kisiasa.


Profesa Mwandosya ni mbunge wa Rungwe Mashariki (CCM). Alikuwa miongoni mwa waliokuwa kwenye mchakato wa kugombea urais mwaka 2005.


Mwingine anayetajwa katika njama hizo ni mwenyekiti wa chama hicho mkoa wa Mbeya, Nawab Mulla. Katika orodha hiyo, yumo pia mkurugenzi wa zamani wa Usalama wa taifa, Cornel Apson Mwang’onda.


Kwa mujibu wa mawasiliano yaliyopo kati ya Profesa Mwandosya, Mwakipesile, Mwalimu wa Shule ya Msingi Lufilyo, Alisto Gideon Mwangungulu na Stephen Merali Mwakajumilo, wafadhili wakuu wa mkakati ni Rostam na swahiba wake Lowassa.


Taarifa zinasema Profesa Mwandosya huenda akagombea urais mwaka 2015, mwaka ambao pia imetajwa kuwa Lowassa angependa kuingia kwenye kinyang’anyiro.


Kuanguka kwa Profesa Mwandosya, taarifa zinaeleza, kunaweza kuwa ni kumsafishia njia Lowassa katika kuwania urais mwaka 2015.


Mwaka 2005 Profesa Mwandosya alikuwa mmoja wa wanachama wa CCM waliotoa ushindani mkubwa kwa rais Jakaya Kikwete katika kinyang’anyiro cha kutafuta mgombea urais kupitia chama hicho.


Tangu wakati huo, taarifa zinasema, kumekuwa na madai ya kutaka kumuangamiza kwa maelezo kuwa anaweza kutamani kugombea tena nafasi hiyo mwaka 2015.


Aidha, taarifa zinasema Mwandosya amekuwa akikabiliwa na upinzani mkali kutoka ndani na nje ya chama, kutokana na kutokuwa mfuasi wa kundi maarufu la “wanamtadao,” lililomuingiza Kikwete madarakani.


Mkakati huo wa siku nyingi umevuja mwezi mmoja uliopita, baada ya Mwalimu Mwangungulu “kuungama” kwa Mwandosya akiwa na viongozi wengine wa dini.


Alisema aliitwa na Mwakipesile na kutakiwa kusaidia harakati za kumtokomeza Mwandosya.


Kwa mujibu wa mawasiliano ya siri kati ya viongozi hao wawili, Mwakipesile, anatuhumu Mwandosya kuwa mtu anayejisikia na asiyethamini viongozi wake wa mkoa na kitaifa.


Mwalimu Mwangungulu anasema katika ungamo lake kwamba Mwakipisile alimueleza, “…Mwalimu ngoja nikuambie yafuatayo: Mbunge wenu ana kiburi, ana dharau. Sijui ni kutokana na elimu aliyonayo?


Anasema, “…Nasema ana dharau na ana kiburi kwa kuwa akitoka Dar es Salaam anatakiwa kuripoti kwangu na wilayani. Yeye huwa anapitiliza moja kwa moja kwenda kijijini kwake Lufilyo.”


Mwangungulu alimnukuu Mwakipesile akisema, “Yeye (Profesa Mwandosya) amemwambia rais anihamishe kutoka mkoa huu, eti sina maendeleo yoyote.”


Alisema, “Mimi ndiye mkuu wa mkoa. Ndiye ninayepanga ratiba ya rais ya mkoa huu. Kwa hali hiyo, Rais Jakaya Mrisho Kikwete hatakanyaga Lufilyo labda niwe marehemu au niwe nimehamishwa kutoka mkoa huu.”


Habari zinasema Mwakipesile aliona kuwa iwapo rais atakwenda kijijini Lufilyo, nyumbani kwa Profesa Mwandosya, basi waziri huyo angeweza kupata ujiko wa kisiasa.


Hata hivyo, Rais Kikwete alifika kijijini hapo mwaka jana baada ya kuombwa binafsi na Profesa Mwandosya wakati huo wakiwa katika ziara ya kikazi nchini Marekani.


“Wakiwa Marekani (Mwandosya na Kikwete), Profesa alimuomba rais atembelee kijijini kwake kwa mwaliko wa mkewe, Mama Mark Mwandosya kwa ajili ya kufungua kituo cha watoto yatima cha Lufilyo. Ndipo Mwakipisile alipotaka kuhujumu ziara hii,” anasema kiongozi mmoja wa serikali aliyeulizwa iwapo anafahamu lolote kuhusiana na suala hilo.


Alisema, “Katika ziara yake ya kwanza mkoani Mbeya baada ya kurejea kutoka Marekani, viongozi wa mkoa hawakumpangia kutembelea Lufilyo. Lakini katika ziara ya pili, rais aliagiza kutoka Dar es Salaam, kwamba anakwenda Mbeya na anataka akifika tu, aende Lufilyo.”


Baada ya maelezo ya Mwangungulu, ndipo Profesa Mwandosya alipochukua hatua ya kumuandikia Mwakipesile kutaka kuweka kile alichoita, “kumbukumbu na matumizi ya baadaye.”


Katika barua yake ya tarehe 16 Aprili 2010, Profesa Mwandosya anasema, “…Naambatanisha kumbukumbu (transcript) ya kikao ulichokifanya (Mwakipesile, Mwalimu Mwangungulu na Mwakajumilo) Jumatatu ya Pasaka 3 Machi 2008 pale Mbeya Hotel. Somo la mazungumzo linajieleza lenyewe…ikiwa ni pamoja na washiriki wengine.”


Anasema kiini cha kupeleka kumbukumbu hizo zinazodaiwa kuandikwa na Mwalimu Mwangungulu, ni ili azipitie “na kufanya marekebisho” atakayoona yanafaa.


Barua ya Mwandosya kwenda kwa Mwakipesile ilikuwa na kichwa cha maneno kisemacho, “Kumbukumbu ya mkutano wa tarehe 3 Machi 2008.” Ilikuwa na Kumb. Na. MJM/JIMBO/RM/02.


Hata hivyo, Mwakipesile hakufanya marekebisho katika waraka wa siri aliotumiwa, badala yake aliandika barua ya kurasa mbili iliyojaa tuhuma, shutuma na lawama kwa Profesa Mwandosya.


Aidha, ni katika barua hiyo, Mwakipesile anaingiza hata watu ambao hawakutajwa mahali popote na Mwalimu Mwangungulu wala na Mwandosya.


Barua ya Mwakipesile ya tarehe 20 Aprili 2010 iliyotumwa kwa Profesa Mwandosya, kwanza inakiri kukutana na Mwalimu Mwangungulu na Mwakajumilo.


Mwakipesile anasema mkutano wao haukulenga kumuangamiza Profesa Mwandosya, bali kuzungumzia maandalizi ya semina ya SACCOS.


Akionyesha hasira katika maandishi yake, Mwakipesile anasema, “Nimeelezwa mengi juu ya masimango yako dhidi yangu, kwamba mimi John Mwakipesile nimemtafuta Mwakajumilo akuondoe ubunge.”


Anasema anadaiwa “…kupokea pesa kutoka kwa Lowassa na Rostam ili nikuondoea ubunge wewe na Mwakyembe. Kwamba mimi, Apson, Mwambulukutu, Mulla mwenyekiti wa CCM mkoa …ni adui zako ambao tuna lengo la kukuondoa uongozi na kuharibu malengo yako ya kisiasa. Unazungumza yote hayo na mengine mbele ya wananchi huko Mwakaleli ambao mimi ni kiongozi wao.”


Mwakipesile anasema, “Sitaki kuingia katika malumbano na wewe. Mimi bado nakuheshimu. Lakini sipendi kuniingiza katika mambo ya kijinga na ya kitoto.”


Akiandika kwa njia ya kumwonya Profesa Mwandosya, Mwakipesile anasema, “Nisingependa tena kuchezewa kiasi hiki.”


Wakati hali ikiwa tete katika jimbo la Mwandosya, Rhoda Mwamunyange, dada mkubwa wa mkuu wa sasa wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), Davis Mwamunyange, amekuwa mwanamke wa kwanza kujitosa kuwania ubunge katika jimbo la Kyela, mkoani Mbeya.


Rhoda ni mfanyakazi wa Shirika la Kazi la Kimataifa (ILO) jijini Dar es Salaam na mtumishi wa siku nyingi wa vyama vya wafanyakazi nchini. Jimbo la Kyela linashikiliwa na Dk. Harrison Mwakyembe.


Wengine wanaotajwa ni George Mwakalinga mjasiriamali na mwanafunzi anayeishi Uingereza na Vincent Mwamakimbula ambaye vilevile ni mjasiriamali anayeishi Dar es Salaam.


Habari kutoka jimbo la Urambo Mashariki zinasema Ali Karavina, ambaye aliwahi kuwa mbunge wa jimbo hilo, ametajwa kujitosa kupambana na mbunge wa sasa, Spika wa Bunge, Samwel Sitta.


Mwingine aliyejitosa kupambana na Sitta ni Ali Kalimauganga.


Taarifa zinasema tayari “kadi feki” 36,000 zimeingiza jimboni humo. Haikufahamika nani ameziingiza, lakini Sitta alipoulizwa kwa simu kutoka Dodoma, alikiri kuwapo kwa kadi hizo na kusema kwa ufupi tu, “Sibabaishwi na majizi.”


Chanzo: Mwanahalisi

Tuesday, June 1, 2010

Serikali yajifilisi !!!!

SERIKALI imeumbuka. Inahaha kukopa fedha benki kujazia bajeti, wakati inatuhumiwa kutumia mabilioni ya shilingi bila maelezo mwafaka.
Taarifa za kuaminika ambazo pia zinathibitishwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), zinauweka utawala wa rais Jakaya Kikwete kitanzini.
Wakati serikali imekopa karibu Sh. 270 bilioni kutoka benki, CAG amethibitisha matumizi mabaya ya serikali yanayofikia Sh. 344.1 bilioni katika mwaka wa fedha uliopita.
Kiasi ambacho CAG anasema kimetumiwa vibaya au bila maelezo mwafaka, kinazidi fedha ambazo serikali inakopa kutoka benki kwa zaidi ya Sh. 74.1 bilioni.
Wiki iliyopita serikali ilisema imekopa Sh. 270 bilioni kutoka benki ya Stanbic ya jijini Dar es Salaam kujazia kwenye bajeti yake ya mwaka 2010/2011.
Hatua hiyo ya serikali inatokana na wafadhili kukata kiasi cha dola za Marekani 220 milioni sawa na Sh. 270 bilioni kutoka kwenye ahadi zao za kusaidia bajeti ya Tanzania kwa mwaka huo.
Wafadhili wameeleza kwamba kiasi hicho kimekatwa kutokana na serikali kutokuwa makini katika kukusanya mapato na kukosa nidhamu katika matumizi. Wameeleza kwamba serikali haitekelezi ahadi zake hasa kuhusu uhuru wa vyombo vya habari na demokrasia kwa ujumla.
Kwa mujibu wa CAG, ofisi ya rais ni miongoni mwa zilizotumia vibaya fedha za serikali. Ripoti inaoyesha kuwa mwaka wa fedha wa 2008/2009 utumishi, iliyo chini ya ofisi ya rais, imetumia vibaya Sh. 282 milioni.
Fedha hizo zimetumika kulipia matumizi ya watumishi wake kulala hotelini, wakati watumishi hao tayari walilipwa na serikali fedha za kujikimu.
Aidha, CAG anasema ofisi hiyo imetumia kiasi cha Sh. 705 milioni bila ya kuwa na nyaraka za kuthibitisha matumizi yaliofanyika.
Katika kile kinachoonekana kuchota kila kinachopatikana, ofisi hiyo ya rais imelipa ofisa wake mmoja kiasi cha Sh. 13.3 milioni ikiwa ni asilimia 30 ya posho ya nyumba, huku akiwa amepewa nyumba na serikali.
MwanaHALISI lilipomuuliza Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC), John Cheyo kuhusu matumizi ya ikulu na mengine ya serikali, alisema “ni mapema mno kuzungumzia suala hilo.”
Alisema, “Sisi tumeipata ripoti hiyo ya CAG kwenye mkutano uliopita wa Bunge na bado hatujaidili. Kwa kweli katika mazingira haya nitakuwa napayuka tu kama nitazungumza lolote.”
Cheyo alisema sharti kamati yake ipate maelezo kamili ndipo iweze kutoa maoni yake.
Wizara nyingine ambazo CAG anasema zimetumia fedha vibaya au bila vielelezo sahihi, ni pamoja na wizara ya elimu na mafunzo ya ufundi.
Katika wizara hiyo, CAG amegundua Sh. 3.6 bilioni zilizohamishwa kutoka fungu la matumizi ya kawaida kwenda katika fungu la ukarabati na manunuzi zilitumiwa vibaya.
CAG anasema katika ripoti yake kuwa, fedha hizo zilizohamishiwa fungu la ukarabati na manunuzi, hazikutumika kwa kazi iliyotajwa.
“…Hakukuwapo na ukarabati wala manunuzi yaliyofanyika. Mpango wa mwaka wa manunuzi na taarifa ya manunuzi, vilionyesha manunuzi hayo hayakufanyika kutokana na ukosefu wa fedha,” anasema CAG.
Matumizi mengine ya kutisha ni yale yaliyofanywa na wizara ya fedha yenyewe. Watendaji wa wizara hiyo, walipeleka kiasi cha Sh. 15 bilioni katika halmashauri mbalimbali ambazo hazikujulikana zilivyotumika.
Fedha hizo zimepelekwa bila ya kufahamisha Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI) jambo lililosababisha “kutumika vibaya” au kuibwa, taarifa inasema.
Ripoti ya CAG inasema serikali ilitumia vibaya takribani Sh. 68 bilioni, ambazo hazikuwapo katika bajeti.
Aidha, serikali imetumia Sh. 23.7 bilioni ambazo zilitumia kuwekea dhamana Shirika la Umeme nchini (Tanesco). Shirika hilo lilishindwa kulipa deni lake na serikali ikalazimika kulilipa.
Lakini, kubwa kuliko yote, ni uamuzi wa serikali kubadili deni la Sh. 135 bilioni kutoka katika Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA) kuwa dhamana itakayolipiwa riba ya Sh. 11.50 kwa mwaka.
Kutokana na uamuzi huo, CAG anasema, “serikali italazimika kulipa kiasi cha Sh. 230 bilioni katika kipindi cha miaka 20 ijayo.”
Matumizi mengine ya Sh. 2 bilioni yamelipwa kwa mifuko ya hifadhi ya jamii inayomiliki kampuni ya M/S Pensions Properties Limited (PPL).
Mifuko hiyo imechotewa na serikali na washirika wake kiasi cha Sh 2, 845, 637,096 kama faini ya ucheleweshaji malipo yaliyotolewa kwa ajili ya ujenzi wa “ukumbi mdogo wa Bunge - Dodoma.”
Mifuko iliyolipwa fedha hizo ni Shirika la Hifadhi ya Jamii (NSSF), Mfuko wa Pensheni wa Mashirika ya Umma (PPF), Mfuko wa Pensheni wa Watumishi wa Serikali za Mitaa (LAPF) na Mfuko wa Pensheni wa Watumishi wa Umma (PSPF).
Kama hiyo haitoshi, CAG anasema serikali imelipa kiasi cha Sh. 4 bilioni kwa wamiliki wa hoteli ya Travertine ya jijini Dar es Salaam, kutokana na kushindwa katika shauri lililofunguliwa mahakamani na menejementi ya hoteli hiyo.
Menejementi ya Hotel Travertine ilifungua kesi Na. 350 ya mwaka 2002 kutokana na serikali kuvunja mkataba wake na hoteli ambao CAG anasema, “haukuwa na manufaa yoyote kwa serikali.”
Serikali pia imepoteza kiasi cha Sh 17.8 bilioni zilizokusanywa na Idara ya Uhamiaji Zanzibar ambazo hazikuwasilishwa katika serikali ya Muungano.
Ripoti hiyo imeeleza pia namna wizara ya fedha ilivyofanya manunuzi makubwa yenye thamani ya Sh 1.6 bilioni ili kuepuka fedha zilizokuwa hazijatumika hadi wakati huo zisirejeshwe kwenye Mfuko Mkuu wa Serikali.
Akizungumza na waandishi wa habari, wiki iliyopita, Waziri wa Fedha na Uchumi, Mustafa Mkulo, alisema mapato ya serikali yameshuka kwa wastani wa asilimia sita.
Mkulo alisema Mamlaka ya Mapato (TRA) haikusanyi kama awali na uuzaji wa bidhaa nje umepungua.
Hata hivyo, Mkulo alijitetea kuwa uchumi wa nchi umeimarika kiasi cha kuwa na nguvu ya kukopa fedha hizo na kwamba hata washirika wa mawandeleo - Benki ya Dunia (WB) na Shirika la Fedha Duniani (IMF) hawana kikwazo kwa maamuzi hayo.
Wakati Waziri Mkulo akipiga siasa katika suala nyeti la uchumi, taarifa zinasema sarafu ya taifa imeporomoka kwa kasi ambayo haijawahi kufikiwa.
Katika kipindi cha wiki moja iliyopita, sarafu hiyo imeshuka thamani yake kwa wastani wa Sh. 60.
Kiongozi mmoja wa ngazi ya juu serikalini aliliambia MwanaHALISI kuwa ripoti ya CAG imeiumbua serikali, kutokana na mabilioni hayo ya shilingi kutojulikana yalivyotumika.
Katika Wizara ya Miundombinu, CAG amekutana na msururu wa madai ya wizara na idara za serikali zilizoagiza magari kupitia wizara hiyo, lakini yakiwa bado hayajafika.
Hata Ofisi ya Msajili wa Vyama imeguswa. Katika hali ambayo haijaweza kutosheleza ofisi ya CAG, msajili ametumia takribani Sh. 17 milioni kumlipia mtumishi wake mmoja fedha za kujikimu wakati wa mafunzo yake ya mwezi mmoja nchini Swaziland.
Kwa upande mwingine, CAG anasema wizara ya Mambo ya Nchi za Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, imefanya manunuzi yenye thamani ya Sh. 103.06 milioni nje ya “mpango wa manunuzi wa mwaka” na bila manufaa.
Aidha, wizara ilitumia kiasi cha dola za Marekani 151,000 kukarabati jengo ililolinunua kwa dola za Marekani 10.5 milioni nchini Marekani, wakati kwa mujibu wa mkaguzi wa majengo, jengo hilo halikustahili kukarabatiwa. habari kwa hisani ya mwanahalisi